ISRAELI KUENDELEA KUTEKAS ARDHI GAZA


  Israel kuendelea kupora ardhi zaidi za Wapalestina

Israel imesema kuwa ina mpango wa kunyakua mamia ya hekta za ardhi katika eneo ililolighusubu la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan. 

Vyombo vya habari vya utawala wa Kizayuni wa Israel vimetangaza kuwa, mpango huo ni sehemu ya miradi ya Tel Aviv ya kuendeleza ujenzi wa vitongoji vya walowezi. Duru za jeshi la Israel zimeripoti kuwa hekta za ardhi karibu ya 400 katika kitongoji cha Gevaot kusini mwa mji wa Bait-laham zimetangazwa kuwa ni ardhi ya Israel.

Wakati huo huo baraza la vitongoji la Israel limekaribisha mpango huo mpya wa kupanua makazi ya walowezi wa Kizayuni na kueleza kuwa mradi huo utafungua njia ya kupanuliwa kitongoji cha Gevaot na pia kuanzisha mji mpya.

 Taasisi isiyo ya kiserikali ya Israel kwa jina la B'Tselem imeeleza kuwa Tel Aviv imepora mamia ya maelfu ya hekta za ardhi kutoka kwa Wapalestina huko katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan tangu mwaka 1967 kwa minajili ya kujenga vitongoji zaidi ya 200 vya walowezi wa Kizayuni.