Siku chache baada ya kusambaa kwa sauti katika mitandao ya kijamii, 
ikiwemo WhatApp na Facebook, inayodaiwa kutengenezwa kwa lengo la 
kumchafua Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe na 
mrembo wa Tanzania mwaka 2006, Wema Sepetu, hatimaye ‘dude’ limeamka na 
sasa kimenuka.
HAPA NDIPO ILIPOANZIA
Mwishoni mwa wiki iliyopita, sauti iliyorekodiwa kama ya watu wanaoongea
 kwenye simu, zilianza kusambaa kwa kasi mitandaoni, ambazo kwa 
kuzisikia harakaharaka, zilionekana kufanana na watu hao wawili, 
zikisikika kama za watu waliokuwa katika uhusiano.
Wakati sauti hizo zinasambaa, muda mchache baadaye, majibizano ya meseji
 kwenye simu yakaanza kusambaa pia, ambayo nayo yanahisiwa kuwa 
yalitengenezwa, yakiwahusisha viongozi wawili wa ngazi za juu katika 
Mikoa ya Arusha na Dar es Salaam, wakipongezana kwa kukamilika vizuri 
kwa kazi hiyo (ya kutenegeneza na kusambaza sauti). Katika majibizano 
hayo ya meseji za simu, ‘viongozi’ hao wawili walimsifu mtu waliyemwita 
Steve (anadhaniwa kuwa Steve Nyerere) kwa kuifanya kazi hiyo vizuri (ya 
kuigiza sauti ya kiongozi huyo).
RISASI LAWASAKA WAHUSIKA
Ili kupata mkanda kamili wa ishu hiyo, Risasi Mchanganyiko liliingia 
mtaani na kuifanyia kazi ili liweze kuwapa wasomaji wake kitu cha 
kueleweka. Freeman Alkael Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema 
Taifa, hakupokea simu aliyopigiwa, lakini wakati Risasi Mchanganyiko 
likienda mitamboni, alisikika kupitia kituo kimoja cha redio jijini 
Arusha, akiikana sauti hiyo na kusisitiza kuwa hajawahi kuwa na uhusiano
 wa kimapenzi na muigizaji huyo na kwamba kinachofanyika ni siasa chafu,
 kitu ambacho kitashughulikiwa na chama.
Wema Sepetu naye simu yake iliita bila kupokelewa na hata baada ya 
kutumiwa ujumbe mfupi, hakujibu licha ya kuonekana kuwa umepokelewa na 
kusomwa.
HUYU HAPA MLEZI WA WEMA CHADEMA
Hata hivyo, Risasi Mchanganyiko lilifanikiwa kumpata mtu aliyepewa 
jukumu la kumlea Wema ndani ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo 
(Chadema), Boniphace Jacob ambaye pia ni Meya wa Ubungo jijini Dar es 
Salaam na hapa anafunguka kuhusu ishu hiyo; “Tumeshaongea na wanasheria 
juu ya hatua kali za kisheria, kuwachukulia hatua
wote wanaoigiza sauti za viongozi wetu na kuzitumia vibaya kwa nia ya 
kuwadhalilisha na kuwashushia heshima, pamoja na kutoa taarifa kwenye 
vyombo vya dola juu ya uchunguzi ufanyike kubaini sehemu na watu 
wanaofanya “voice studio” kwa lengo ovu.
“Pili tumemtia moyo kamanda wetu Wema kuwa asihofu na siasa za majitaka 
na kwamba yote yanafanyika na wapinzani wetu, kwa sababu wanamuhofia na 
kumuogopa
juu ya namna anavyofanya mikakati ya kufuta
“UTUMWA WA WASANII KWA CCM”
kazi ambayo ameifanya na mpaka sasa ameandaa ujio wa wasanii wakubwa 20 ndiyo maana wanataka kumuondoa nje ya agenda yake.”
STEVE NYERERE NAYE AFUNGUKA
Steve Nyerere ambaye kwa mujibu wa meseji zilizoenezwa mtandaoni 
alionekana kama ndiye aliyeshughulika kutengeneza sauti hiyo ya kiume, 
aliruka kimanga kuhusika na suala hilo, aliloliita la kijinga na 
kipumbavu. “Mimi sihusiki, sikutengeneza ile sauti kwa vile sina sababu 
ya kufanya hivyo,
hicho ndicho ninachoweza kukuambia ila kwa nyongeza tu, niwatake 
Watanzania waachane na kufuatilia mambo ya kijinga na kipumbavu, tuna 
vitu vingi sana vya kufanya badala ya kukuza vitu kama hivi.”
SASHA NAYE AZUNGUMZIA ‘SAUTI YAKE’
Sasha, msanii ambaye hutumika kama video queen kwenye nyimbo mbalimbali za Bongo Fleva, ambaye
amefanana sauti kwa kiasi kikubwa na Wema Sepetu, anahusishwa kutumika 
kutengeneza sauti ya kumuigiza malkia huyo wa filamu Bongo. “Nimetumika 
kuiga sauti ya Wema? Hapana, sijawahi kupigiwa simu na mtu yeyote na 
wala sijafanya kitu kama hicho, nikuambie ukweli kuwa hili jambo ndiyo 
kwanza wewe unaniambia, sijui kabisa,” alisema msanii huyo.
TUNDU LISU ABEZA
Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lisu ambaye pia ni Mbunge wa Singida 
Mashariki, alipotakiwa kulizungumzia suala hilo, alisema ni propaganda 
dhaifu, zilizolenga kumchafua mwenyekiti wao, ambayo imeshindwa. “Lengo 
lao lilikuwa ni kumchafua mwenyekiti wetu, lakini hawajaweza kwa sababu 
hawezi kuchafuka kwa staili hii. Tunajua hili jambo hata tukilipeleka 
polisi ni kama kujisumbua tu, hawana historia ya kushughulikia shida za 
wapinzani.”
HAWA HAPA POLISI MAKOSA YA MTANDAO.
Risasi Mchanganyiko lilimpata mmoja wa maofisa wa kitengo cha makosa ya 
mtandao, ambaye alijitambulisha kwa jina moja la Fadhil, akisema yeye 
siyo msemaji wa suala hilo. “Ila ninachoweza kukusaidia kwa hili ni 
kwamba Cyber Crime haifanyi kazi pasipo kupokea malalamiko. Hao ambao 
sauti zao unasema zimeigwa, wanatakiwa waje kulalamika hapa na hapo 
ndipo polisi watakapoanza kufuatilia suala hilo. “Lakini kama wenyewe 
watakaa kimya bila kulalamika, basi suala hilo litaishia kama lilivyo, 
endapo watakuja suala hilo litafanyiwa kazi mara moja,” alisema

