Waziri Mkuu wa Lesotho Thomas Thabane ameondolewa madarakani na
jeshi.
Thabane ambaye kwa sasa amekimbilia nchi jirani ya Afrika Kusini,
amesema kuwa kitendo hicho cha kuondolewa madarakani kilichotekelezwa
na jeshi la nchi hiyo hapo jana kinakinzana na matakwa ya wananchi.
Thomas Thabane pia alikitaja kitendo hicho kuwa ni aina fulani ya
mapinduzi ya kijeshi.
Kwa mujibu wa ripoti, mapema jana milio ya risasi
ilisikika Maseru, mji mkuu wa nchi hiyo ndogo ya kifalme inayozungukwa
na Afrika Kusini, ambapo vikosi vya jeshi vilichukua udhibiti wa makao
makuu ya polisi na kuzingira nyumba ya Waziri Mkuu.
Inaelezwa kuwa
kamanda mkuu wa jeshi la nchi hiyo alikuwa anakusudia kumtia mbaroni
waziri mkuu huyo na naibu wake na kuwakabidhi kwa mfalme.
Hii ni katika
hali ambayo wakati Thomas Thabane anayataja matukio ya hivi karibuni
kuwa ni mapinduzi ya kijeshi, msemaji wa jeshi la nchi hiyo kwa upande
wake, mbali na kukadhibisha habari za kutokea mapinduzi ya kijeshi
ametangaza kuwa, hatua ya kuvinyang'anya silaha vikosi vya polisi,
ilikuwa ni kwa minajili ya kuzuia umwagikaji damu na machafuko ambavyo
vingeweza kutokea ndani ya nchi hiyo.
Pamoja na hayo hivi karibuni
Waziri wa Michezo wa Lesotho, Thesele Maseribane mbali na kutangaza
kudhibitiwa makao makuu ya jeshi la polisi, alielezea pia kuwepo
uwezekano mkubwa wa kutokea mapinduzi ya kijeshi nchini humo.
Hayo
yanajiri katika hali ambayo hatua ya hapo awali ya kugawana madaraka na
kuundwa baraza la mawaziri kwa ushiriki wa vyama mbalimbali, ilileta
matumaini ya kupatikana maendeleo na ustawi ndani ya nyoyo za raia.
Karibu miaka miwili iliyopita, baada ya chama cha Waziri Mkuu wa Lesotho
cha All Basotho Convention
(ABC) kuungana na baadhi ya vyama vya upinzani, kilifanikiwa kutwaa
uongozi wa taifa hilo.
Awali Lesotho ilikuwa ikiongozwa na waziri mkuu
wa zamani, Pakalitha Mosisili aliyeongoza nchi hiyo kwa miaka 14 na
ambaye alikuwa mwanachama wa chama tawala cha wakati huo cha Kongresi ya
Kidemokrasia. Katika uchaguzi uliopita, Mosisili hakufanikiwa kutwaa
ushindi wa kura nyingi, huku chama chake kikipata viti 40 kati ya viti
vyote 80 katika bunge la taifa.
Wakati huo huo pia baadhi ya vyama vya
siasa vikakataa kujiunga na chama cha Kongresi ya Kidemokrasia. Suala
ambalo lilifungua uwanja wa kuingia madarakani Thomas Thabane.
Thabane
aliunda chama chake cha All Basotho Convention
(ABC) "Basotho" hapo mwaka mwaka 2006, ambacho ni tawi lililomeguka
kutoka chama cha Kongresi ya Lesotho kwa ajili ya Demokrasia.
Muda
mchache baadaye chama chake kiligeuka kuwa chama kikubwa mashuhuri cha
upinzani dhidi ya serikali iliyokuwa madarakani wakati huo.
Kwa kutumia
udhaifu wa Mosisili, Thabane akafanikiwa kujiongezea mapenzi ya
wananchi. Mosisili alikuwa akituhumiwa kuwa anawapa nyadhifa muhimu
serikalini watu wa kabila lake na hivyo kuonekana mtu mwenye ukabila.
Mbali na hilo, umasikini uliokithiri katika kipindi cha utawala wake,
ulipelekea kuongezeka manung’uniko ya wananchi dhidi ya kiongozi huyo.
Ni wakati huo huo ndipo jina la Thabane likapata umashuhuri kufuatia
kaulimbiu yake ya kupambana na umasikini na kuinua uchumi wa Lesotho.
Hatimaye sambamba na kupata ushindi wa viti 26 katika bunge, akafanikiwa
pia kupata nafasi ya pili katika uchaguzi.
Muungano wa vyama viwili vya
upinzani vya Kongresi ya Lesotho kwa ajili Demokrasia na chama cha
Kitaifa cha Basotho, uliandaa mafanikio ya Thabane na hivyo kupelekea
kupata viti vingi bungeni na hivyo ikawa sababu ya yeye kutakiwa aunde
serikali.
Pamoja na hayo tangu awali baadhi ya weledi wa mambo waliuhisi
muungano wa vyama hivyo kuwa ni wenye kusuasua.
Hivi sasa kuondolewa
madarakani Waziri Mkuu wa nchi hiyo, kumepunguza sana kiwango cha
matarajio juu ya kustawi demokrasia ndani ya nchi hiyo ya kusini mwa
Afrika.