NI MIAKA 20TENA ILI KUIJENGA GAZA UPYA

Shirika moja la kimataifa linaloshiriki katika mpango wa kulijenga upya eneo la Ukanda wa Gaza baada ya mashambulio ya kinyama ya utawala wa Kizayuni wa Israel limetangaza kuwa unahitajika muda wa miaka 20 kwa ajili ya kulikarabati eneo hilo.

 Shirika la Shelter Cluster ambalo linaendeshwa kwa pamoja na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi UNHCR na mashirika ya Msalaba Mwekundu na Hilali Nyekundu limeripoti kuwa, katika mashambulio ya utawala wa Kizayuni dhidi ya Gaza, jumla ya nyumba elfu 17 zilibomolewa au kuharibiwa vibaya na nyengine elfu tano ziliharibiwa kwa kiwango kidogo cha kuhitajia matengenezo.

Shirika la Shelter Cluster limeongeza kuwa makadirio ya muda wa ukarabati yanategemea uwezo wa vivuko vikuu vya kupitishia vifaa vilivyoko baina ya Gaza na ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu ambapo makadirio yaliyofanywa ni kupitishwa kila siku malori mia moja ya vifaa vya ujenzi kuelekea Gaza.

Wakati huo huo Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa hivi sasa eneo la Ukanda wa Gaza lina uhaba wa nyumba elfu 75 za kuishi.

 Ikumbukwe kuwa mbali na Wapalestina wapatao 2,150 waliouliwa shahidi, katika mashambulio ya kinyama ya utawala wa Kizayuni dhidi ya Gaza yaliyoanza tarehe 8 Julai hadi 26 Agosti maelfu ya nyumba, zaidi ya misikiti 80, zaidi ya shule 140 na majengo 350 ya viwanda na karakhana yalibomolewa…/