SOMALIA YALALAMIKIA HITILAFU YA MIPAKA YAKE NA KENYA



  Hitilafu za mpaka kati ya Kenya na Somalia


Serikali ya Somalia jana iliwasilisha malalamiko kwa Mahakama ya Kimataifa ya Uadilifu, kwa ajili ya kutatua hitilafu zilizopo kati yake na Kenya.

 Viongozi wa Somalia wametaka kuanishwa kwa makini mipaka ya baharini kati ya nchi hiyo na Kenya.

Mjadala uliopo sasa kati ya nchi mbili hizo juu ya haki ya kuchimba mafuta na mapato yanayotokana na maliasili hiyo katika maeneo yenye mafuta kwenye mipaka ya majini, umezidisha wasiwasi wa kuibuka mapigano.

 Kwa mujibu wa barua ilitowasilishwa na Somalia katika Mahakama ya Kimataifa ya Uadilifu, mazungumzo yaliyofanywa na nchi mbili hizo hadi sasa yameshindwa kutatua hitilafu zilizopo.

Hitilafu za mpaka kati ya Somalia na Kenya si suala jipya.

 Nchi mbili hizo kwa miaka kadhaa sasa zimekuwa zikivutana kuhusu akiba ya mafuta katika bahari ya Hindi.

 Hitilafu kati ya Kenya na Somalia pia zimeyaathiri makampuni ya mafuta ya nchi kadhaa yanayoendesha shughuli zao katika eneo la mashariki mwa Afrika.

Weledi wa mambo wanaamini kuwa, katika hali ambayo Somalia inakabiliwa na tatizo la maharamia, mchafuko ya ndani, vitisho vya kundi la al Shabab, jeshi dhaifu na uwezekano wa kutokea tena janga la njaa nchini humo, vita kati ya nchi hiyo na majirani zake, ni changamoto mpya ambayo inaweza kuyafanya maisha ya raia wa Somalia kuwa magumu zaidi.

 Pamoja na hayo yote na licha ya kuweko matatizo ya aina mbalimbali, wapembuzi wa mambo wanasema hatua yoyote ya kusalimu amri serikali ya Mogadishu mbele ya haki zake katika maji ya Bahari ya Hindi inakinzana na maslahi ya nchi hiyo.

 Hasa ikitiliwa maanani kwamba, madola makubwa ya eneo hilo na yale ya mbali yamepanga mikakati ya kuwa na udhibiti katika maji ya bahari hiyo kutokana na kuweko maliasili muhimu hususan maliasili na akiba ya nishati jadidika katika Bahari ya Hindi.

Bahari ya Hindi ni bahari ya tatu kwa ukubwa duniani. Bahari hiyo ni pia mlango la kuingilia bahari saba muhimu za dunia na milango bahari minne ya kistratejia yaani Hormoz, Babul Mandan, Malaka na Suez.

 Zaidi ya asilimia 40 ya biashara ya kimataifa inapita katika mlango bahari wa Malaka na asilimia 40 ya mafuta ghafi yanayozalishwa duniani hupitia katika mlango bahari wa Hormoz. 

Wakati huo huo asilimia 60 ya  bidhaa na biashara ya kimataifa hufanyika kupitia Bahari ya Hindi.

 Imeelezwa kuwa, hadi kufikia mwaka 2030, mahitaji ya nishati ya dunia yataongezeka kwa asilimia 45.

Usafirishaji wa asilimia 70 ya mafuta duniani kupitia Bahari ya Hindi ni ishara ya umuhimu wa bahari hiyo katika suala la nishati duniani.

 Weledi wa mambo wanaamini kuwa, kupenda makuu na tabia ya kujitanua ya baadhi ya nchi vinavuruga na kuharibu mazingira ya ushirikiano.

 Vilevile ni wazi kuwa miongoni mwa sababu muhimu za kuwepo ustawi katika nchi za kanda hiyo ni kujiepusha na mizozo na hitilafu.

 Kwani kuwepo hitilafu na mgawanyiko kutayapa madola ya kikoloni fursa ya kuingia tena katika eneo hilo na kupora maliasili zake.

Kwa msingi huo ilitarajiwa kwamba nchi jirani za Kenya na Somalia zilipaswa kuketi chini na kutafuta suluhisho la amani la mgogoro wa mpaka wa majini na hivyo kuzuia uwezekano wa aina yoyote wa kuyapa fursa madola ya kikoloni.