WANAJESHI ZAIDI YA 20 WA CAMEROON WAMEUAWA NA BOKO HARAM


Duru za jeshi la Cameroon zimeripoti kuwa, zaidi ya wanajeshi 20 wa nchi hiyo wameuawa katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita katika vita dhidi ya wanamgambo wa Boko Haram.

 Duru hizo zimetangaza kuwa, wanajeshi 25 wa Cameroon wameuawa katika kipindi cha mwezi mmoja kufuatia mapigano ya jeshi la nchi hiyo na kundi la wanamgambo wa Boko Haram wenye makao yao nchini Nigeria. 

 Taarifa zaidi zinasema kuwa, wanajeshi hao wameuawa katika mapigano huko kaskazini mwa Cameroon ambapo kunashuhudiwa kuongezeka mashambulio ya Boko Haram.

Katika miezi ya hivi karibuni, jeshi la Cameroon limeanzisha vikosi vipya na kutuma vikosi vya kuongeza nguvu katika maeneo ya kaskazini mwa nchi hiyo kwa shabaha ya kupambana na wanamgambo wa Boko Haram wanaoripotiwa kuendesha operesheni za mashambulio katika maeneo hayo.

 Pamoja na hayo serikali ya Cameroon inalaumiwa na wapinzani na wananchi wengi wa nchi hiyo kutokana na kushindwa kukabiliana na wanamgambo wa Boko Haram.