Baraza la Ushirikiano wa Ghuba ya Uajemi (GCC) na ndoto za umiliki wa visiwa vya Iran


Baraza la Ushirikiano wa Ghuba ya Uajemi (GCC) na ndoto za umiliki wa visiwa vya Iran
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa taarifa iliyotolewa na Baraza la Ushirikiano wa Ghuba ya Uajemi (GCC) kuhusu visiwa vitatu vya Iran vya Tombu Kubwa, Tombu Ndogo na Abu Mussa inaonesha jinsi nchi wanachama wa baraza hilo zisivyoelewa uhakika wa historia na hali ya sasa ya eneo hili.

Bi Marziyeh Afkham amesema, taarifa hiyo ni kielelezo cha wazi cha kuingilia mambo ya ndani ya Iran na kwamba Tehran mbali na kulaani taarifa hiyo inasisitiza kuwa, misimamo kama hiyo haina faida yoyote na inapotosha fikra za watu na kuchelewesha ushirikiano wenye faida kati ya nchi za Ghuba ya Uajemi.

Mwishoni mwa mkutano wao wa Jumamosi iliyopita huko Jiddah, Saudia Arabia, Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi za GCC walitoa taarifa wakidai kuwa visiwa hivyo vitatu yaani Tombu Kubwa, Tombu Ndogo na Abu Mussa si milki ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran

. Katika vikao vyake vya huko nyuma pia Baraza la Ushirikiano wa Ghuba ya Uajemi limekuwa likidai kuwa visiwa hivyo vitatu ni milki ya Umoja wa Falme za Kiarabu, nchi ambayo iliundwa mwaka 1971 wakati visiwa hivyo vilikuwa katika milki ya Iran hata kabla ya kuundwa nchi hiyo.

Mawaziri wa Mambo ya Nje wa GCC ambao walilazimika kukutana Jiddah kwa sababu ya kujadili tishio la ugaidi na kutatua tofauti zao za ndani, walighafilika na asili ya mjadala na kucheza tena karata butu.

Uzoefu wa miaka 33 ya tangu kuundwa Baraza la Ushirikiano wa Ghuba ya Uajemi umeonesha kuwa, baraza hilo linaundwa na nchi zisizo na uwiano na zenye mitazamo tofauti ambazo hazikuweza kutibu majeraha ya miaka mingi; kwa msingi huo zinatumia uchochezi kwa ajili ya kuficha udhaifu wao.

 GCC linaingilia mambo ya ndani ya Iran kwa kukariri madai ya umiliki wa visiwa vitatu vya Iran wakati ushahidi na nyaraka za kimataifa zilizothibitishwa na Umoja wa Mataifa zinaonesha kwamba, visiwa hivyo ni milki ya Iran.

Mshauri wa Chuo Kikuu cha Umoja wa Mataifa Pirouz Mujtahizadeh anasema: Nyaraka saba zimetiwa saini kuhusu visiwa vitatu vya Iran na hata serikali ya Imarati ambayo ni miongoni mwa nchi wanachama wa baraza la GCC imetia saini nyaraka hizo.

Kwa kuzingatia nyaraka na hati hizo madhubuti inadhihiri kwamba, kwa kukaririwa madai hayo kuhusu visiwa vitatu vya Tombu Kubwa, Tombu Ndogo na Abu Mussa katika vikao mbalimbali, GCC imeazimia kuingilia mambo ya ndani ya Iran kwa kutumia madai yasiyo sahihi kuhusu visiwa hivyo vya Iran na kupuuza ujirani mwema.

Kung’ang’ana na msimamo huo wa kupotosha historia na kutegemea nyaraka zisizo sahihi hakuwezi kulifikisha baraza la GCC kwenye malengo yake.

 Kuheshimiana na ujirani mwema ndiyo mambo yanayopaswa kuwa msingi wa ushirikiano kati ya nchi za eneo hili la Ghuba ya Uajemi na ushirikiano huo unaweza kuwa msingi wa kumaliza ukosefu wa maelewano likiwemo suala la visiwa hivyo vitatu.


Kwa upande wao viongozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran wamekuwa wakisisitiza mara kwa mara kwamba, siasa za Tehran kuhusu majirani zake hususan nchi za kando ya Ghuba ya Uajemi, zimejengeka juu ya ujirani mwema, kuheshimiana na kujiepusha na hatua yoyote ya kuingilia masuala ya ndani ya nchi nyingine.