MPANGO WA SERA YA ISRAEL KUJIPANUA WAPINGWA NA JAMII YA KIMATAIFA


  Jamii ya kimataifa yapinga sera za kujipanua za Israel huko Palestina


 Mpango wa utawala wa Kizayuni wa Israel wa kupora hekta mia nne za ardhi za Palestina katika Ukingo wa Magharibi umekabiliwa na upinzani mkubwa katika uga wa kieneo na kimataifa.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban K-moon ameeleza wasiwasi wake kuhusu suala hilo na kusema kuwa ni utangulizi wa ujenzi wa vitongoji vipya vya walowezi wa Kizayuni. 

Ban amesema ujenzi wa vitongoji vya walowezi katika ardhi ya Ukingo wa Magharibi huko Palestina ni kinyume cha sheria za kimataifa na ameutaka utawala wa Kizayuni kutilia maanani matakwa ya jamii ya kimataifa na kuheshimu majukumu yake ya kimataifa.

Baadhi ya nchi za Magharibi pia zimechukua msimamo kama huo wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na kuitaka Israel isitishe mpango wa kutwaa ardhi zaidi za Palestina.

 Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza ameeleza kusikitishwa na mpango wa Israel wa kutaka kupora hekta 400 za ardhi za kusini mwa ardhi za kusini mwa Bait Laham katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na kusema hatua hiyo inakiuka sheria.

 Philip Hammond amesema ujenzi wa vitongoji vipya unakiuka sheria za kimataifa na ni kikwazo kikubwa katika njia ya mazungumzo ya kufikia mapatano baina ya Israel na Wapalestina

. Hammond amesema Uingereza inaitaka Israel itupilie mbali uamuzi wake wa kutwaa ardhi za Palestina katika eneo la Bait Laham.

Utawala wa Kizayuni wa Israel umekuwa ukipora ardhi za Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi kwa zaidi ya miongo sita sasa na kujenga vitongoji vya walowezi wa Kizayuni katika maeneo hayo.

 Uporaji wa ardhi za Wapalestina na kuwalazimisha kuhama makazi yao ni miongoni mwa siasa zinazotumiwa na utawala ghasibu wa Israel kwa ajili ya kubadili muundo wa kijamii wa maeneo ya Wapalestina na kujenga vitongoji vya walowezi.

 Siasa hizo daima zinapingwa na makundi ya mapambano ya ukombozi ya Palestina.

Kuhusu hatua ya sasa ya utawala wa Kizayuni ya kupora hekta 400 za ardhi za Ukingo wa Magharibi, harakati ya Hizbullah ya Lebanon imetoa taarifa ikisema kuwa, njama hiyo inafanyika kwa shabaha ya kukamilisha mpango wa kuiyahudisha Palestina.

Taarifa ya Hizbullah imesema: Wakulima wa Kipalestina, baba na mababu zao wamekuwa wakitumia ardhi hizo kwa miaka mingi kwa ajili ya kilimo cha zaituni lakini sasa utawala ghasibu wa Israel umeghusubu maeneo hayo na kuyaunganisha na ardhi nyingine zinazokaliwa kwa mabavu kwa shabaha ya kutekeza njama zake za kubadili muundo wa jamii ya Ukingo wa Magharibi.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Misri pia imelaani hatua hiyo ya Israel na kusema, kutwaa ardhi hizo za Palestina kunakiuka makubaliano ya kimataifa na maamuzi ya Kamati ya Pande Nne ya Kimataifa.

 Taarifa ya Wizara hiyo imesema uamuzi huo ni hatua hasi katika mchakato wa eti amani ya Mashariki ya Kati na kwamba suala hilo linaweza kuwa na taathira mbaya.

 Baadhi ya wataalamu wa mambo wanasema Israel imechukua hatua hiyo ya kughusubu hekta 400 za ardhi za Palestina kwa shabaha ya kuficha kushindwa kwake huko Ghaza baada ya kufikiwa makubaliano ya kusitisha vita na harakati ya Hamas.

 Hata hivyo harakati za mapambano za Palestina zinasema kuwa jibu la uvamizi huo mpya wa Israel ni kudumisha mapambano dhidi ya maghasibu Wazayuni.          

Chanzo;Idhaa ya Kiswahili ya Radio Iran