DUNGA AENDELEA NA USHINDI BRAZIL





Brazil, chini ya himaya mpya ya Kocha Dunga, walitawala, walitamba na kuwachakaza Wenyeji wao Turkey kwa Bao 4-0 ndani ya Atatürk Olimpiyat Stadı Jijini İstanbul kwenye Mechi ya Kimataifa ya Kirafiki iliyochezwa Jumatano Usiku.
 
Brazil walipata Bao lao la kwanza Dakika ya 20 baada ya pasi ndefu ya Fernandinho kushushwa kifuani na Neymar na kuambaa nayo ndani ya Boksi na kuachia shuti lililomshinda Kipa Demirel



Bao la pili la Brazil lilifungwa Dakika ya 24 baada ya krosi ya Fulbeki wa Kulia, Danilo, kuguswa na Beki wa Uturuki Kaya na pengine kumparaza Sentafowadi wa Brazil Luis Adriano na kutinga.

Hata hivyo, Bao hilo liliandikwa kama ni Goli la kujifunga wenyewe Mfungaji akiwa Kaya.
Neymar alifanya kazi kubwa na ufundi mkubwa kwa kuihadaa ngome ya Uturuki na ngoma kumfikia Willian aliefunga na kuipa Brazil Bao la 3 katika Dakika ya 44.

Hadi Mapumziko Uturuki 0 Brazil 3.

Dakika ya 61, uchawi wa Neymar ulionekana tena baada ya kufunga Bao safi alipolishwa Winga ya kushoto na kutumbukia ndani ya Boksi na kuihadaa Difensi nzima ya Uturuki na kufunga Bao la 4 kwa utaalam mkubwa.

Matokeo haya yanaendeleza uteja wa Uturuki kwa Brazil kwani wameshakutana mara 6 na Brazil kushinda Mechi 5 na Sare moja ya 0-0 Mwaka 2007.

Pia, himaya mpya ya Kocha Dunga imeendelea kwa wimbi la ushindi wa Mechi zake zote 5 tangu atwae madaraka mara baada ya kumalizika Fainali za Kombe la Dunia huko Brazil kwa kuzitandika pia Colombia, Ecuador, Argentina na Japan huku wakifunga jumla ya Bao 12 bila kufungwa hata moja na Neymar akipiga Bao 7 kati ya hizo.

Mechi inayofuata kwa Brazil ni hapo Jumanne Novemba 18 huko Vienna watakapocheza na Wenyeji wao Austria.

VIKOSI VILIVYOANZA:
Turkey (Mfumo 4-4-2): Demirel; Kaya, Irtegun, Koybasi, Tufan; Altintop, Topal, Kisa, Turan; Bulut, Erding.

Brazil (Mfumo 4-3-3): Diego Alves; Danilo, Miranda, David Luiz, Filipe Luis; Luiz Gustavo, Fernandinho, Oscar; Willan, Luiz Adriano, Neymar