VIGOGO CCM NUSURA WAZICHAPE HADHARANI

Katibu wa CCM mkoa wa Singida, Mary Chatanda

Vigogo wawili wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wilayani hapa nusura wazichape  hadharani baada ya kutoleana maneno ya kashfa.   
Vigogo hao ni Katibu wa CCM mkoa wa Singida, Mary Chatanda ambaye pia ni Mbunge wa Viti maalumu na Katibu wa CCM Wilaya ya Korogwe, Mwanaidi Mbisha.
 
Kufuatia tukio hilo, makada wa chama hicho wilayani Korogwe wamelaani na kusema limewaondolea sifa viongozi hao.
Wametishia kuandamana kama chama  hakitachukua hatua dhidi yao kwani licha ya viongozi hao kujifedhehesha lakini pia wamekidhalilisha chama.
 
Mmoja wa makada hao ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini alidai chanzo cha ugomvi huo ni Chatanda kumtuma kijana mmoja (jina linahifadhiwa) kumnunulia maziwa kwa kutumia gari la Mbisha bila kumjulisha mwenyewe.
 
Alisema baada ya Mbisha kuona gari lake linatoka bila idhini yake, alitoka nje na kuhoji nani aliyeamua kuchukua gari lake bila ruhusa yake wakati funguo akiwa nazo yeye. 
 
Ilidaiwa kuwa baada ya Mbisha kuhoji ndipo Chatanda alipodakia na kuanza kumtolea mwenzake maneno ya kashfa.
 
Kada huyo alisema nyumba ya Chatanda na Mbisha zimekaribiana.  “Ukweli pale yalikuwapo maneno makali sana huyu mama Chatanda akimtukana mwenzake kumuita masikini, fukara huku akisema anaweza kumhamisha na maneno mengine si busara kutaja. Wakati huo wote Mbisha alikuwa akitaka kujua gari lake liliondokaje wakati funguo yake anayo,” alisema kada huyo.
 
Inadaiwa kuwa licha ya chanzo cha ugomvi kuwa ni gari lakini jimbo ndiyo linalogombewa. “Pale kuna siasa tena zile chafu, Chatanda anatarajia kuwania ubunge sasa anahisi kwamba Mbisha hawezi kumuunga mkono katika lengo lake hilo hivyo alikuwa akimshughulikia angalau aweze kusalimu amri, lile la gari lilijitokeza tu,” alisema kada mwingine.
 
Kufuatia patashika hiyo, Mbisha alilazimika kupiga simu polisi na baada ya kufika walimkuta Chatanda akiendelea kufoka.
 
Habari kutoka vyanzo vya habari ndani ya polisi zinasema waliutatua mgongano huo baada ya kuthibitisha kuwa funguo zilizotolewa zinatumika kufungua gari lingine.
 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Frasser Kishai, alikiri kutokea kwa tukio hilo.
 
Mbisha alipohojiwa na gazeti hili alisema Oktoba 30, majira ya saa 2.25 asubuhi akiwa nyumbani kwake alisikia gari lake likiwashwa na alipomtuma kijana wake kufuatilia, kijana aliyetoka na gari alimjibu amepewa funguo na katibu wa CCM Korogwe vijijini, Jumanne Kitundu na hapo ndiyo chanzo cha kutukanwa na Chatanda.
 
“Yule mama licha ya kunitolea matusi mazito hadharani, lakini alinitishia kunifukuzisha kazi na kuhoji vipi sijahamishwa wakati alishafanya mipango ya kuhamishwa katika wilaya hiyo…,” alisema Mbisha.
 
Naye Chatanda alipoulizwa kwa njia ya simu kuhusu tukio hilo, alijibu kwa mkato kwamba  hana maelezo kwa jambo ambalo halifahamu.
 “Mimi sijui chochote, habari za Mbisha, muulize Mbisha mwenyewe… Mbisha ni Mbisha na mimi ni Chatanda sawa," alisema na kukata simu.
 Hata hivyo, katibu wa  CCM Mkoa wa Tanga, Shijja Othuman, alipoulizwa alidai kuwa hana taarifa.
CHANZO: NIPASHEA