YANGA WASEMA MSUVA ATAUZWA NJE


Baada ya klabu mbili za ligi kuu ya Bara wakiwemo watani wa jadi Simba kutangaza kumuhitaji winga hatari Simon Msuva, Yanga imesema mchezaji wake huyo ni wa hadhi ya kuuzwa nje ya nchi tu kama timu hiyo itaamua kufanya hivyo.
 
Simba imetangaza kumuhitaji winga huyo ambaye ameonyesha kiwango cha juu tangu mwaka jana huku akionekana kuwa mkombozi wa Yanga msimu huu.
 
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, kocha msaidizi wa Yanga Salvatory Edwarad alisema hawafikirii kumuuza Msuva kwa kuwa ni mmoja wa wachezaji muhimu kwenye kikosi hicho.
Alisema ana uhakika "wakubwa" wake wa kazi hawatafikiria kumuuza nyota huyo kwa klabu za ligi kuu na kama itatokea ulazima wa kufanya hivyo labda kwa ofa kutoka nje ya nchi.
 
"Hayo ni maneno ya tu ambayo tunayasikia lakini Msuva ni mchezaji mkubwa na muhimu (hivyo) kamwe Yanga haitafikiria kumuuza kwa kipindi hiki; tena kwa timu ya ligi kuu," alisema.
Vyombo mbalimbali vya habari vimewanukuu baadhi ya viongozi wa Simba wakisema watapeleka barua Yanga kwa ajili ya kutaka kumsajili winga huyo hatari.
 
Msuva ambaye pia yupo kwenye kikosi cha timu ya taifa 'Taifa Stars', amekuwa akionyesha kiwango kikubwa kwenye kikosi cha Yanga.
Hivi karibuni kocha mkuu Marcio Maximo aliiambia Nipashe kuwa nyota huyo ni hazina kwa taifa na mmoja wa wachezaji muhimu kwenye kikosi chake.
 
Katika mchezo uliopita wa ligi kuu ya Bara dhidi ya Mgambo JKT, Msuva aliingia kutoka benchini katika kipindi cha pili na kufunga mabao mawili yaliyoipa timu yake ushindi wa 2-0.
Kwa sasa viongozi wa Yanga wapo makini na karibu na mchezaji hiyo ili kuhakikisha harubuniwi na timu pinzani, uchunguzi wa Nipashe umegundua.
CHANZO: NIPASHE