Shirika
la ujasusi la Marekani FBI huko Ohio limemkamata mwanamume mmoja kwa
kupanga njama ya kufanya shambulizi katika eneo la Capitol ambako makoa
ya baraza la Congres yapo, mjini Washington.
Stakabadhi za
mahakama zinasema kuwa mwanaume huyo aliyetajwa kuwa Christopher Cornell
mwenye umri wa miaka 20 , alikuwa amejaribu kununua bunduki akitaka
kumuua afisaa mmoja mkuu wa serikali.
Shirika la FBI lilimtambua baada ya kugundua kwamba alikuwa ametuma ujumbe wa Twitter kuunga mkono kundi la wapiganaji wa kiisilamu la IS na vita vya jihad akitumia jina bandia la Raheel Mahrus Ubaydah.
Hata hivyo wananchi hawakua katika hatari ya kushambuliwa wakati wa uchungizi, alisema afisaa mmoja wa FBI.
Babake Cornell anasema mwanawe huenda alituma ujumbe kuhusiana na vita vya jihadi lakini hakuwa na uwezo wa kufanya mashambulizi ya kigaidi.
John Cornell aliambia shirika la habari la ABC kwamba mwanawe amesilimu tu hivi karibuni baada ya kupoteza mwelekeo wa maisha yake akiwa shule ya upili.
Bwana Cornell alisisitiza kwamba mwanawe hakuwa na uwezo wa kupanga njama ya mashambulizi ya kigaidi kwani katika maisha yake hajawahi kuzungumzia ghasia au vurugu au hata mashambulizi ya aina yoyote.
Christopher Cornell alikamatwa kwa kununua silaha mnamo siku ya Jumatano, na amekuwa akichunguzwa na maafisa wa ujasusi.
Inadaiwa alikuwa na akauti ya Twitter ambayo, aliitumia kwa jina jengine la Raheel Mahrus Ubaydah, ambayo maafisa wa ujasusi walitambua na kuanza kumshuku mnamo mwezi Agosti.